DKT. MWIGULU NCHEMBA WAZIRI KUU MPYA TANZANIA, WABUNGE WAMPITISHA, ASUBIRI KUAPISHWA NA RAISI

 


Wabunge wamemthibitisha Dokta MWIGULU NCHEMBA, kuwa Waziri Mkuu Mteule wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Kura 369 kati ya Kura 371 zilizopigwa.

Jina hilo lilithibitishwa kwa kupigiwa Kura baada ya kupendekezwa na Rais Dokta Samia Suluhu Hassan.

Akitangaza matokeo leo Bungeni Katibu wa Bunge Baraka Leonard amesema kati ya Kura zilizopigwa, 2 zimeharibika na hakukuwa na Kura ya hapana.

Akisoma wasifu, Mwanasheria Mkuu wa Serikali Hamza Johari amesema Dokta Nchemba ni Mchumi mbobevu mwenye Shahada ya Uzamivu katika masuala ya Uchumi.

Amesema Dokta Mwigulu ana uwezo wa kuchambua na kupima hoja mbalimbali na upeo wake mpana umejidhihirisha katika utumishi wake wa Umma.

Waziri Mkuu Mteule wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dokta Mwigulu Nchemba, ametoa wito kwa watanzania kuhakikisha Taifa linaendelea kuwa na Amani.

Akifafanua amesema yote yaliyo katika Dira, Ilani ya CCM na matamanio ya watanzania, yatatimia kama Taifa litaendelea kuwa na Amani.

Aidha amesema ni lazima maono ya Rais Dokta Samia Suluhu Hassan na ahadi zitekelezwe.

Pia ametumia nafasi hiyo kusema Serikali inatambua mahitaji ya watanzania na itaendelea kutatua Kero zao.

Dokta Mwigulu ametumia nafasi hiyo kukemea Wala Rushwa, Wavivu, Wazembe na kusema watachukuliwa hatua.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dokta Samia Suluhu Hassan, alipendekeza jina la Dokta Mwigulu Nchemba ambaye ni Mbunge wa Iramba Magharibi kuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Dokta Nchemba anarithi kiti cha aliyekuwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa.

Jina la Dokta Nchemba, limeletwa leo Bungeni na mpambe wa Rais na kutangazwa na Spika wa Bunge Mussa Azzan Zungu.

Dokta Nchemba amewahi kushika nafasi mbalimbali nchini ikiwemo Naibu Waziri wa Fedha, Waziri wa Kilimo, Waziri wa Mambo ya Ndani, Waziri wa Sheria na Katiba na amewahi kuwa Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi Bara.

Nafasi ya mwisho aliyokuwa nayo kabla ya kurudi Bungeni baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025, ni Waziri wa Fedha.

wakimzungumzia Dokta Mwigulu baadhi ya Wabunge akiwemo Mbunge wa Mkoani Pemba Profesa Makame Mbarawa, wamesema Dokta Mwigulu ni wa kipekee.

Naye Mbunge wa Peramiho Jenista Mhagama amesema Dokta Nchemba ni Jasiri na msimamizi anayetaka mambo yatokee.

Mbunge wa Same Mashariki Anne Kilango amesema Dokta Mwigulu anafikika huku Mbunge wa Tunduru Kaskazini Ado Shaibu ameeleza ana imani Dokta Mwigulu atasimamia vizuri katika usimamizi wa Rasilimali za Taifa katika kuleta Maendeleo.

No comments