NCHI INAWEZA KUJIENDESHA BILA MISAADA - MSIGWA

Baada ya ongezeko la wasiwasi kuhusu mustakabali wa msaada wa kimataifa kufuatia matukio ya Oktoba 29, msemaji wa Serikali ya Tanzania, Gerson Msigwa, ametolea ufafanuzi uhusiano wa Tanzania na wahisani, akisisitiza kuwa nchi inaweza kuendelea kusimama kwa miguu yake bila misaada, ingawa amekiri kupungua kwake huzua mtikisiko.

Katika mahojiano yake na mwandishi wa habari Edwin Odemba, Msigwa alieleza kuwa asilimia kubwa ya bajeti ya taifa inatokana na makusanyo ya ndani, hivyo misimamamo ya baadhi ya wahisani haitaiangusha Tanzania. "Mwaka huu bajeti yetu ni shilingi trilioni 56, kati ya hizo, trilioni 40 zinatokana na makusanyo yetu wenyewe. Misaada katika bajeti ni trilioni 1.07 tu," alisema.

Kwa mujibu wake, mikopo inayochangia shilingi trilioni 14 katika bajeti ni fedha ambazo "tunachukua na tunalipa", tofauti na misaada ambayo huweza kukatwa au kucheleweshwa kwa misingi ya kisiasa au kidiplomasia.

Alisisitiza kuwa takwimu hizo zinaonyesha nchi haitong'ang'ania msaada ili kuendelea kufanya kazi zake. "Ukiangalia hizi takwimu unaona hatuwezi kushindwa. Kama trilioni 55 ni za kwetu, tutakwama wapi?"

No comments