MBAMBA BAY BANDARI KUFUNGUA FURSA ZA BIASHARA YA MAFUTA
Ujenzi wa Bandari ya Mbamba Bay unatarajiwa kuchochea kwa kiasi kikubwa biashara ya mafuta katika ukanda wa Kusini na kufungua njia mpya za usafirishaji wa bidhaa hiyo kuelekea nchi jirani kupitia miundombinu ya kisasa inayojengwa eneo hilo.
Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa bandari hiyo, Meneja wa Mipango ya Mafuta wa Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA), Gilbert Jungulu, amesema mradi huo una nafasi ya kuifanya Tanzania kuwa kitovu muhimu cha usambazaji wa mafuta kwa nchi za Malawi, Msumbiji na maeneo mengine ya ukanda huo.
Amesema PBPA itaendelea kuratibu uagizaji wa mafuta nchini pamoja na kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha miundombinu muhimu ya mafuta, ikiwemo maghala ya kuhifadhia mafuta, inajengwa na kuimarishwa ili kurahisisha biashara ya kikanda.
Kwa upande wake, Mhandisi Mkazi wa mradi huo, Agathon Mwenda, amesema bandari inajengwa kwa kiwango cha kisasa ikiwa na uwezo wa kuhudumia magari na mizigo kwa wakati mmoja, pamoja na kupokea meli zenye uwezo wa kubeba hadi tani 5,000.




Post a Comment