WATAALAM 1649 TIBA ASILI TABORA, WAITIKIA WITO WA SERIKALI KUJISAJILI



Msajili wa tiba asili na Tiba  Mbadala Bi. Lucy Mziray amesema kuwa, mkoa wa Tabora umeitikia wito wa Serikali uliotolewa hivi karibuni na Waziri wa afya Mhe. Mohamed Mchengerwa kwa wataalam na  watoa  huduma za tiba asili na Tiba mbadala kujisajili na kupata leseni, kwa  lengo la kuboresha utoaji wa huduma hiyo muhimu kwa jamii ya Watanzania 


Hayo yamesemwa Aprili 28, 2026 mkoani Tabora wakati wa kuhitinisha zoezi la utoaji wa elimu na usajili wa papo kwa papo  wa Wataalam hao, amsema lengo lilikuwa kusajili wataalam wa tiba asili 1000 katika Mkoa wa Tabora  lakini waliosajiliwa wamevuka lengo na kufikia  1649 ikiwa ni ongezeko la asilimia 60, amesema mwitikio umekuwa mkubwa kwa Wilaya zote nane walizopita na Wilaya ya Nzega imekuwa kinara katika zoezi hilo.


Bi.Lucy Mziray amesema kuwa zoezi hilo ni endelevu, kwani serikali imepanga kuanzia mwezi Julai, 2026, zoezi la usajili  litaendelea katika mikoa ambayo zoezi halijafanyika kwa lengo la kuhakikisha wataalam wote wa tiba asili wanatambulika kwenye mifumo rasmi ya afya lengo la usajili ni kuhakikisha jamii inapata huduma kwa wataalam ambao huduma zao zinatambulika.


“Naomba kutoa wito kwa jamii ya Watanzaniakupata huduma za tiba asili na tiba mbadala kwa wataalam waliosajiliwa, kwani wataalam hawa wanafuata maadili na miiko ya utoaji wa huduma bora kwa wananchi,tujiepushe na matapeli wachache wasiojisajili, Bi.Mziray


Aidha,ameongeza kuwa,baada ya zoezi kukamilika mkoani hapo kitakachofuata ni zoezi la ufuatiliaji na utozaji wa faini mbalimbali pamoja na kuchukua hatua za kisheria kwa wale wanatoa huduma bila kusajiliwa.


Bi. Mziray pia  ametoa shukrani kwa  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Waziri wa Afya kwa usimamizi bora na maelekezo aliyoyatoa ya kuhakikisha wataalam wa tiba asili nchini wanasajiliwa karibu na maeneo wanapoishi.


Naye mnufaika wa huduma ya usali wa tiba asili Bw.Daniel Charles kutoka Wilaya ya Kaliua mkoa wa Tabora  ametoa pongezi nyingi kwa Rais Samia pamoja na Waziri wa Afya kwa kusogeza huduma ya usajili wa wataalam wa tiba asili hadi ngazi za chini.


Kwa upande wake,mratibu wa Tiba asili na Tiba mbadala mkoa wa Tabora Bi.Nyabawela Mahuyu,ameishukuru Wizara ya Afya kupitia Baraza la Tiba asili kwa kuleta huduma ya mkoba hadi mkoa wa Tabora kuanzia tarehe 8-28 Aprili, 2026, amewashukuru wataalam wa Tiba asili kwa kuitikia wito na kujitokeza kwa wingi katika wilaya zote nane na  kujisajili.


Aidha, ametoa ombi kwa  Wizara ya Afya na Baraza la Tiba asili na Tiba mbadala kuendelea kuja mkoa wa Tabora na kuendesha zoezi kama hilo.









No comments