WAZIRI GWAJIMA AKEMEA UVUMI WA KUPOTEA KWA NYETI, AITAKA KUPUUZIA IMANI HIZO POTOFU
Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima, amekemea vikali uzushi unaoenezwa na baadhi ya watu wenye nia ya kupotosha jamii kuwa mwanaume akishikwa bega hupoteza sehemu zake za siri (Nyeti)
Dkt. Gwajima amekemea uzushi huo Aprili 12, 2026, wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Mtoto Anayeishi na Kufanya Kazi Mtaani yaliyofanyika katika Wilaya ya Ubungo, mkoani Dar Es Salaam, yaliyolenga kuhamasisha ulinzi, malezi na ustawi wa watoto.
Maadhimisho hayo yamehudhuriwa na Mhe. Angelah Kairuki , Mbunge wa Kibamba na Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari pamoja na viongozi wa kisekta, Mkoa, wilaya na wadau wa Maendeleo wakiwemo Shirika la SOS, RCA Tanzania, UVIWADA, UMAWATA na watoto tunu yetu na Makundi mengine ya kijamii.
Akizungumzia uzushi huo, Dkt. Gwajima aliendesha zoezi la wanaume kushikana mabega, wakiongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Mhe. Albert Msando, ili kuthibitisha ukweli wa madai hayo ambapo mara baada ya zoezi hilo, wanaume walithibitisha kuwa taarifa hizo ni za uongo, kwani hakuna aliyepotelewa nyeti zake.
Aidha, Dkt. Gwajima amewataka wananchi kupuuza uzushi huo na badala yake wajikite katika shughuli za maendeleo na ustawi wa jamii huku akisisitiza umuhimu wa kujenga jamii yenye uelewa sahihi inayoweza kupambanua taarifa za kweli na za upotoshaji ili kuimarisha maendeleo endelevu ya taifa.
Katika hatua nyingine, Dkt. Gwajima amewaelekeza viongozi wa Wizara hiyo kuongeza juhudi za utoaji wa elimu kwa jamii ili kuondoa dhana potofu hiyo, akisisitiza kuwa upotoshaji wa aina hiyo unalenga kupunguza umakini wa wananchi katika ajenda za maendeleo na ustawi wa jamii.
Post a Comment