NEMC NA ZEMA ZAIMARISHA USHIRIKIANO USIMAMIZI NA UHIFADHI WA MAZINGIRA NCHINI
Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) na Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira Zanzibar (ZEMA) wameimarisha ushirikiano wao kuingia makubaliano ya pamoja ya usimamizi na uhifadhi wa mazingira nchini.
Makubaliano hayo yamefikiwa katika kikao cha siku mbili kilichofanyika kuanzia tarehe 7 hadi 8 Oktoba 2025, ambapo wajumbe wa Bodi na wataalamu kutoka taasisi zote mbili walikutana kujadiliana na kubadilishana uzoefu kuhusu utekelezaji wa majukumu yao.
Kupitia kikao hicho, taasisi hizo zimeweka msingi wa ushirikiano madhubuti katika maeneo mbalimbali, yakiwemo matumizi ya teknolojia ya kidijitali katika usimamizi wa mazingira, ufuatiliaji wa utekelezaji wa sheria na Kanuni za mazingira, pamoja na kuimarisha mawasiliano ya mara kwa mara kati ya pande hizo mbili.
Aidha wamekubaliana pia kuhakikisha kuwa miradi yote inayotekelezwa upande wa Tanzania Bara na Zanzibar inazingatia mchakato wa Tathmini ya Athari kwa Mazingira (EIA).
Akizungumza na vyombo vya habari, Mwenyekiti wa Bodi ya NEMC, Mhandisi Mwanasha Tumbo, amesema ushirikiano huo ni hatua muhimu kuelekea utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2020/2050, ambayo inaweka mazingira kama mojawapo ya nguzo kuu za maendeleo ya Taifa.
Amesisitiza kuwa mashirikiano hayo yataongeza ufanisi katika utendaji kazi na kusaidia kufanikisha malengo ya kitaifa ya uhifadhi wa mazingira kwa maslahi ya wananchi na vizazi vijavyo.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya ZEMA, Bi. Asha Ali Khatib, amesema kikao hicho kimetoa fursa kwa wataalamu wa pande zote mbili kujifunza kutoka kwa wenzao, na pia kuibua mbinu mpya za kuboresha utendaji.
Ameongeza kuwa ushirikiano huu utawezesha uwiano wa kisera na kiutekelezaji katika masuala ya mazingira baina ya Tanzania Bara na Zanzibar.






Post a Comment