MNDOLWA ATANGAZA MKAKATI MPYA WA KUSAFIRISHA MITAMBO YA VISIMA VIREFU

 


Tume ya Taifa ya Umwagiliaji -NIRC imeanza kuweka mikakati ya jinsi ya kusafirisha mitambo yake mikubwa ya kuchimba visima virefu kwenda maeneo mbalimbali nchini, hususani yale yenye changamoto kubwa ya upatikanaji wa maji chini ya ardhi, mara baada ya kukamilisha kazi katika shamba la Chinangali. 


Mkurugenzi Mkuu wa NIRC, Raymond Mndolwa, ametoa agizo hilo kwa Idara ya Mitambo, ya Tume hiyo kutathmini namna bora ya kusafirisha mitambo hiyo bila kuathiri miundombinu ya barabara kutokana na uzito wake mkubwa. 


Agizo hilo amelitoa wakati wa ziara yake katika shamba la vijana la mradi wa Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) lililopo Chinangali mkoani Dodoma. 


Ziara hiyo ililenga kukagua maendeleo ya ujenzi wa barabara za ndani, mabwawa,uchimbaji wa visima na uwekaji wa miundombinu ya Umwagiliaji katika mashamba hayo,inayotekelezwa na Tume hiyo. 


Katika ziara hiyo, Mndolwa alikagua mtambo huo wa kisasa wenye uwezo wa kuchimba visima virefu hadi mita 1,800 chini ya ardhi, ambao kwa sasa upo Chinangali kwa ajili ya kuchimba visima viwili vya mwisho. Visima hivyo vitakamilisha jumla ya visima 40 vinavyochimbwa na NIRC shambani hapo, sambamba na mabwawa matatu ambapo mawili tayari yamekamilika ili kuongeza kasi ya upatikanaji wa maji.








No comments