WAANDISHI WA HABARI WAPIGWA MSASA UTAYARISHAJI VIPINDI VYA WATOTO
Waandaaji wa vipindi vya watoto wamehimizwa kutumia taaluma zao na lugha rafiki kwa watoto na vijana pamoja na kuzingatia maadili ya taaluma ya Habari katika kuandaa maudhui yenye ubora yatakayochangia ukuaji na maendeleo ya mtoto katika jamii.
Hayo yamesemwa na Mratibu wa Programu ya malezi na familia kutoka Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Victor RugalabamuMei 8, 2026 wakati wa kuhitimisha mafunzo maalum yaliyoandaliwa na Wizara hiyo kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto (UNICEF) kwa lengo la kuwajengea uwezo waandaaji wa vipindi wa radio za jamii, Televisheni na Mitandao ya Kijamii katika kutengeneza maudhui yanayofundisha, kuburudisha na kuhamasisha maadili mema kwa watoto.
Victor amesema, kupitia mafunzo hayo, Wizara inatarajia kuona vipindi vitakavyorushwa kupitia vyombo vya habari vinatoa mafunzo ya maadili mema kwa kizazi cha sasa na kijacho pia vinahamasisha malezi mazuri ndani ya familia na kuwasaidia watoto na vijana balehe kukua katika mazingira salama, yenye upendo na ulinzi.
Kwa upande wake Mwezeshaji wa mafunzo hayo, Sabrina Majikata kutoka Shirikia Lisilo la Kiserikali la ICS amesema mafunzo yamejikita kuwawezesha Waandishi wa Habari katika kutayarisha vipindi bora na kuzungumza kwa ufasaha katika nguzo tatu ambazo ni namna ya mzazi kumjali, kumtunza na kuzungumza na mtoto ili aweze kubaini changamoto zinazoweza kuathiri maendeleo yake.
“Mwandishi wa habari anapokuwa na uelewa kuhusu ukuaji wa watoto na changamoto zinazowakabili pamoja na vijana balehe, anakuwa na uwezo mkubwa wa kutengeneza maudhui yenye manufaa kwa jamii.
Kupitia mafunzo haya, tumesisitiza umuhimu wa kuandaa vipindi vinavyolinda maslahi ya mtoto, vinavyotoa elimu sahihi na vinavyochochea mawasiliano mazuri ndani ya familia”. Amesema Sabrina
Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF) Alice Mwiru ambaye ni Mtaalamu wa mabadiliko ya tabia za jamii, amehimiza waandishi wa habari kuongeza ubunifu na uwajibikaji katika utayarishaji wa vipindi vya Watoto, amesisitiza kuwa UNICEF itaendelea kushirikiana na Serikali kuboresha maudhui yanayohusu watoto ili kuhakikisha haki za mtoto na masuala yao yanapewa kipaumbele katika majukwaa ya habari.
Naye mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo Godliver Thomasi kutoka Jamii Forums amesema mafunzo hayo yamempa mwanga zaidi namna ya kuandaa vipindi husika.
“Mafunzo haya yamenipa uelewa mpana kuhusu namna ya kuandaa maudhui yanayowagusa watoto na vijana kwa njia sahihi na yenye kujenga. Nimejifunza umuhimu wa kutumia lugha rafiki, kuzingatia hatua za ukuaji wa mtoto pamoja na kuandaa vipindi vinavyofundisha na kuburudisha kwa wakati mmoja. Kupitia elimu hii, ninaamini nitakuwa sehemu ya kuleta mabadiliko chanya katika jamii kupitia kazi yangu ya uandishi wa habari”.










Post a Comment